Alhamisi 4 Juni 2026 - 19:55
Khomeini Mkuu na shahidi Khamenei walihuisha utayari wa taifa

Hawza/ Mtukufu Ayatullah Sayyid Mujtaba Husseini Khamenei amesema: Khomeini Mkuu na shahidi Khamenei waligundua na kuhuisha utayari wa taifa.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, ujumbe wa Mtukufu Ayatullah Sayyid Mujtaba Husseini Khamenei, Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu, kutokana na mnasaba wa Idi ya Ghadir na kumbukumbu ya miaka thelathini na saba ya kufariki kwa Imam Khomeini (r.a), na pia kumbukumbu ya mwaka wa kuanza uongozi wa Mtukufu Ayatullah Shahidi Sayyid Ali Khamenei, ulisomwa leo asubuhi katika Haram ya Imam Marehemu na Hujjatul-Islam Muhammad Jawad Haj Ali Akbari.

Matini kamili ya ujumbe huu ni kama ifuatavyo:

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu

“Sifa zote ni za Mwenyezi Mungu ambaye amejaalia ukamilifu wa dini Yake na ukamilifu wa neema Yake kupitia uongozi wa Amirul-Muuminina Ali bin Abi Talib as.”

Nawapongeza Waislamu wote na wanaompenda baba wa Umma wa Kiislamu, Amirul-Muuminina Ali swalatullahi wa salamuhu alayh, nchini Iran na duniani kote kwa Idi tukufu ya Ghadir, na ninaituma salamu na dua kwa roho takatifu ya Imam Khomeini rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Mwaka huu ni tarehe 14 Khordad ya thelathini na saba tangu kupita kwa kuondokewa na Khomeini Mkuu, na pia ni tarehe ya kwanza ya 14 Khordad tangu baba mwenye upendo wa umma, mfuasi na msaidizi mwaminifu na mashuhuri wa madhehebu ya Imam, Kiongozi mkuu shahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Mtukufu Ayatullah al-Udhma Sayyid Ali Khamenei, Mwenyezi Mungu ainue hadhi yake tukufu, awe mgeni katika karamu ya Mwenyezi Mungu, na sauti yake yenye uimara mkubwa pamoja na maneno yake ya hekima na yenye ushawishi mkubwa yasisikike tena katika kaburi tukufu la Imam.

Lakini mkusanyiko wa hotuba na maandiko ya miaka kumi ya mwanzilishi wa Jamhuri ya Kiislamu na miaka thelathini na sita ya Kiongozi mkuu shahidi ni hazina yenye thamani kubwa na isiyo na mfano kwetu sisi sote, na ni nuru inayoongoza njia ya siku zijazo.

Kwanza, leo ni Idi ya Ghadir na Idi kubwa zaidi ya Mwenyezi Mungu; siku ya ahadi iliyokubaliwa na mkataba uliopokelewa ambapo Mwenyezi Mungu alibainisha jukumu la usimamizi wa jamii na mfumo wa Kiislamu, na akaukamilisha Uislamu na neema Yake kupitia wilaya na uimamu endelevu wa Maimamu watakatifu wote, swalatullahi alayhim ajmaiin.

Ghadir humkumbusha yule ambaye kila wakati wa maisha yake matukufu tangu mwanzo wa kuzaliwa kwake ndani ya Kaaba hadi kufikia daraja ya shahada, alikuwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na katika njia ya Mwenyezi Mungu.

Kwa msingi huo, baada ya kuwepo Mtume wa Mwenyezi Mungu (saww), mtukufu huyo katika nyakati zote za maisha na kwa Waislamu na Waumini wote, huhesabiwa kuwa kigezo cha juu kabisa na mfano kamili; na ni jambo linalostahili na linalopasa kwamba kuanzia watoto wadogo mpaka wazee, na kutoka kwa watu wa kawaida wa jamii hadi wasomi na viongozi, wamfuate mtukufu huyo; kama ambavyo fahari ya maisha ya Maimamu wawili wa Mapinduzi pia ilikuwa ni kumfuata mtukufu huyo.

Pili, leo ni kumbukumbu ya kuaga dunia Imam wa Umma, rehema za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na ni fursa yenye thamani kwa ajili ya kutafakari na kujadiliana kuhusu shakhsia hii mashuhuri lakini isiyojulikana kwa undani.

Ni shakhsia yenye mvuto mkubwa ambayo ufahamu na utambuzi wa kina wa njia yake na lengo lake lenye nuru ni taa ya kuongoza mustakabali wa Iran, lakini watu wengi wa taifa ambao wako katika umri wa ujana hawakupata fursa ya kumfahamu moja kwa moja, na hata wengi waliopata zama za maisha yake, hawakufikia undani wa shakhsia yake na njia ya Imam.

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:


قُلۡ إِنَّمَاۤ أَعِظُكُم بِوَ ٰ⁠حِدَةٍۖ أَن تَقُومُوا۟ لِلَّهِ مَثۡنَىٰ وَفُرَ ٰ⁠دَىٰ


"Sema: Hakika mimi ninakunasihini kwa jambo moja tu: msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu wawili wawili au mmoja mmoja."
[Surah Sabaʾ: 46]

Mwenyezi Mungu Aliyetukuka na Mtakatifu katika aya hii tukufu anamwambia Mtume (saww): Waambie umma kwamba mimi nawapa mawaidha kwa jambo moja tu, nalo ni kwamba msimame kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, wawili wawili au kila mmoja kivyake.

Aya hii tukufu ndiyo mwanzo wa ujumbe wa kwanza na moja kati ya nyaraka za kale kabisa ambamo shakhsia ya kipekee ya mja mwema na roho kubwa ya zama na wakati wetu, Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi na mwanzilishi wa Jamhuri ya Kiislamu, ndani yake aliliita taifa la Iran kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.

Ndiyo, kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (Qiyam lillah) ndiyo msingi wa madhehebu ya Imam, na miongoni mwa athari muhimu kabisa na baraka za uwepo wake ni kuiongoza, kuilea na kuiathiri kwa namna kubwa jamii kwa msingi wa msingi huo huo.

Harakati hii ya Kimungu ndiyo chanzo cha kushuka kwa baraka na maangalizi ya Mola, na kutekelezwa kwa sunna ya Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kuiongoza jamii kwenye njia ya haki, kama asemavyo:

وَالَّذِينَ جَاهَدُوا فِينَا لَنَهْدِيَنَّهُمْ سُبُلَنَا

"Na wale waliofanya juhudi kwa ajili Yetu, hakika Tutawaongoza katika njia Zetu."

Je, si kweli kwamba harakati muhimu zaidi za kijamii na mwamko wa taifa la Iran katika zama za Imam Khomeini Mkuu na Khamenei mtukufu shahidi zimetokea kwa uongozi wao wa moja kwa moja au usio wa moja kwa moja?

Ni nguvu gani kubwa ambayo ingeweza kuliamsha taifa lililokuwa limelala na kurogwa na ubeberu na ukoloni katika mazingira ambayo kufungwa kwa njia zote, ukandamizaji na utegemezi kamili kwa Magharibi vilikuwa vinatawala, katika tarehe kumi na tano Khordad mwaka 1342?

Ni nguvu gani ya mvuto ingeweza kuwavuta mamilioni ya watu tarehe kumi na mbili Bahman mwaka 1357 kwa ajili ya mapokezi, na tarehe kumi na nne Khordad mwaka 1368 kwa ajili ya kumuaga Imam wa Umma, hadi kumiminika mitaani?

Na katika mfano wa mwisho wa kushangaza, ni nguvu gani thabiti na azma ya chuma iliyolilifanya taifa la Iran tangu alfajiri ya tarehe kumi Esfand mwaka 1404 kuinuka namna hiyo na kuingia uwanjani kwa motisha ya juu, licha ya kupita zaidi ya miezi mitatu, bado linaendelea kwa hamasa kubwa kudai damu ya kiongozi wake shahidi na mashahidi wengine waliolala katika damu zao, na kuilinda heshima ya mfumo wa Kiislamu na nchi yao pendwa, likiwa bado lipo uwanjani na kuimarisha safu za makumi ya mamilioni wanaojitolea maisha yao kwa ajili ya kutimiza malengo ya kiongozi shahidi, kusimamisha haki na kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu?

Ndiyo, hawa walikuwa ni Khomeini Mkuu na Khamenei mtukufu shahidi ambao waligundua na kufufua kipaji na utayari huu ndani ya taifa pendwa la Iran, na daima walikuwa wakilipa thamani maalumu jambo hili.

Imam mtukufu ambaye bila shaka, kwa uchamungu wake wa mfano, alikuwa makini sana na yale yaliyokuwa yakitoka katika maneno yake, katika wasia wake alitoa dai kubwa na akaandika hivi: "Mimi kwa ujasiri nasema kwamba; taifa la Iran na mamilioni ya watu wake katika zama hizi ni bora kuliko taifa la Hijaz katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu (saww), na taifa la Kufa na Iraq katika zama za Amirul-Mu’minin na Hussein bin Ali, amani na salamu za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao wawili."

Leo hii taifa lote pendwa linajivunia kwamba kupitia mwamko wake mpya, sambamba na mhimili wa muqawama, limekuwa sababu ya fahari mbele ya macho ya watu wenye uelewa na mataifa huru duniani, na kwa mara nyingine limeudhihirisha ukweli wa sehemu hii ya wasia wa Imam Khomeini.

Kwa maelezo ya kiongozi shahidi — Mwenyezi Mungu aitukuze zaidi hadhi yake tukufu — ule mkono wenye nguvu ambao uliweza kuifanya bahari kubwa ya taifa kutibuka kwa mawimbi makubwa ulikuwa ni shakhsia ya chuma, moyo uliotulia na ulimi wenye nguvu mfano wa Dhulfiqar ya Imam mtukufu na Khomeini Mkuu; ambaye aliweza kuwaingiza mamilioni ya watu uwanjani, kuwabakisha uwanjani na kuwafundisha mwelekeo wa harakati.

Na bila shaka mfano mwingine wa aina hii ya athari ni wa Khamenei mpendwa mwenyewe, ambaye alifuata njia ya mtangulizi wake mwema, na kwa takribani miongo minne ya uongozi wa mapinduzi na mfumo wa Kiislamu, kwa kuwaamini vijana na kwa kuimarisha na kuinua kiwango cha ufahamu na mtazamo wa watu, aliifikisha jamii kwenye kiwango cha utayari kiasi kwamba baada ya tukio kubwa la shahada yake, kiwango kipya cha mwamko wa taifa la Iran kilijitokeza.

Ndiyo, madhehebu ya Khamenei mpendwa ni yale yale ya Khomeini Mkuu katika mwendelezo wa Uislamu halisi wa Muhammad (saww), ambao msingi wake ni kusimama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, na wanafunzi wa madhehebu haya wako safu kwa safu tayari kusimamisha haki, kuondoa batili na kufanya jihadi katika njia hii yenye nuru.

Imam — Mwenyezi Mungu amrehemu — ndiye aliyeleta mabadiliko makubwa ya kihistoria katika kiwango cha Iran, Umma wa Kiislamu na dunia; na kiongozi shahidi — Mwenyezi Mungu aitukuze zaidi hadhi yake tukufu — alijishughulisha na kuyakuza, kuyapanua na kuyaendeleza, na kwa ajili ya kuyakamilisha na kuyatekeleza alijenga mfumo na jamii.

Katika mwelekeo huu, mtukufu huyo, mbali na kuendeleza uhai wa madhehebu ya Imam kwa kauli, maandishi na vitendo, na katika mikutano yake mbalimbali, aliifanya tarehe kumi na nne Khordad kuwa fursa ya ahadi ya kila mwaka ya taifa kwa Imam Khomeini, na alikuwa akieleza na kufafanua mfumo wa misingi, sera na mielekeo ya madhehebu ya Imam.

Miongoni mwa baadhi ya mafundisho hayo ambayo huenda yalikuwa yakirudiwa mara kwa mara ni kwamba: taifa la Iran ni taifa lenye imani, lenye akili na lenye ujasiri; na kwamba watu ndio wamiliki wa kweli wa nchi na ndio chanzo cha nguvu yake; na kwamba watu hawa wanaweza kuleta mabadiliko yoyote sahihi watakayoyafuata na wanaweza kuifanya kaulimbiu ya “Sisi tunaweza” kuwa halisi katika nyanja mbalimbali.

Mafundisho mengine ni ulazima wa kumuunga mkono mwenye kudhulumiwa kama wajibu wa Kiislamu, kibinadamu na wa Kiirani. Na kwamba mfumo wa utawala wa mabavu, ambao Marekani iko juu yake, una tatizo na taifa hili pamoja na utambulisho wake wa kipekee na msimamo wake wa kutokusalimu amri.

Ndio, mfumo wa utawala wa mabavu ambao umetengeneza kambi ya kijeshi iitwayo Israeli takribani miaka themanini iliyopita, haukubali kuwepo kwa Iran yenye nguvu, huru na yenye aina mbalimbali za manufaa katika mpaka wa mashariki wa jiografia ya uongo na isiyo na msingi ya “Israeli Kubwa”, yaani mashariki ya Mto Frati; na hauachi juhudi yoyote katika kuzuia maendeleo yake.

Katika nafasi hii napenda pia kuliambia taifa pendwa kwamba; adui mwovu sasa baada ya kushindwa katika makabiliano yake dhidi ya watoto wenu mashujaa walioko katika vikosi vya ulinzi, na hasa kutokana na kukutana na pigo kali katika mapambano ya kijeshi pamoja na katika medani na mitaani, amepata fedheha yenye maana kubwa na ya kina, ambayo matokeo yake yamesababisha mataifa kujitenga naye kwa namna inayoonekana.

Kutokana na hali hiyo, sasa ameelekeza hila zake katika vita mchanganyiko kwenye maeneo mawili:

Kwanza: uwezo wa watu kuvumilia na kustahimili;

Pili: kusababisha makosa katika mfumo wa mahesabu ya viongozi wa nchi.

Silaha yake kuu katika mambo haya yote mawili ni kupanda mbegu za hofu, kukata tamaa, woga, kudhaniana vibaya na kuleta mifarakano.

Kwa hiyo, katika kukabiliana na uovu huu, ni lazima watu wote kwa pamoja, kwa kusimama imara, kuwa na mwangaza wa uelewa, kuhifadhi umoja, mshikamano, kuaminiana na kutoungana na adui, wavuruge na kuharibu mpango wake mwovu.

Katika jambo hili, nafasi ya viongozi katika kusaidia mambo haya ni muhimu sana.

Hatua yoyote inayosababisha watu kuwa na mtazamo mbaya au kuvunjika moyo kwa wananchi, huhesabiwa kuwa ni aina ya msaada kwa adui wa nchi hii na watu wake.

Sasa fursa mpya imepatikana kwa ajili ya kuitambulisha kwa vitendo na kuyatekeleza madhehebu ya Khomeini Mkuu na Khamenei mpendwa shahidi kama viongozi waliodhulumiwa lakini wenye nguvu, na bila shaka washindi wa Mapinduzi ya Kiislamu duniani kote.

Jukumu hili muhimu liko juu ya mabega ya watu wote wa taifa, hususan vijana, wasomi na watu wa fikra, elimu na sanaa, ili kwa msingi wa madhehebu haya, kwa kuamini ahadi za Mwenyezi Mungu, chini ya kivuli cha uangalizi wa kiongozi wetu — Mwenyezi Mungu aharakishe faraja yake tukufu — na katika njia ya Uislamu halisi, yaani njia yenye nuru iliyochorwa katika kipindi cha miaka mia mbili na hamsini ya uwepo wa wenye Isma na Wilayah Kubwa — amani na salamu za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao wote — wajenge mustakabali wenye kung'aa wa Iran pendwa.

Namuomba Mwenyezi Mungu Muweza wa yote alilifikishe taifa hili lililofufuliwa, kwenye ushindi wa mwisho na vilele vya utukufu, maendeleo na ukuu; na roho tukufu za Maimamu wa Mapinduzi pamoja na roho safi za mashahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu, hususan mashahidi wa utetezi mtakatifu wa pili na wa tatu, azikusanye pamoja na kiongozi wao, Amirul-Mu’minin Ali — amani na salamu za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Na moyo mtakatifu na wenye nuru wa kiongozi wetu, Imam wa zama, uridhike na taifa la Iran; na taifa hili pendwa pamoja na watumishi wake wawe miongoni mwa wanaonufaika na dua zake maalumu na uombezi wake, kwa fadhila na ukarimu Wake.

Na amani iwe juu yenu pamoja na rehema za Mwenyezi Mungu na baraka Zake.

Sayyid Mujtaba Hosseini Khamenei
14 Khordad 1405/ 4 June 2026

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha